Blogger Widgets

Tuesday, 24 December 2013

Wanaotesa kwa kutumia miguu ya kushoto Ligi Kuu England

LIGI Kuu England kwa miaka mingi tu imeshuhudia vipaji vya uhakika vya wachezaji wanaotumia miguu ya kushoto. Baada ya Mjerumani Mesut Ozil kutua Arsenal, huku Gareth Bale akihamia Hispania, bado kwenye ligi hiyo kuna wachezaji wanaotisha kwa ufundi wa kutumia miguu ya kushoto.
5. Moussa Dembele - Tottenham
Mbelgiji mwenye uwezo mkubwa wa kutamba kwenye safu ya kiungo na msumbufu wa wapinzani. Kwenye kulifanya hilo, silaha kubwa ya staa huyo ni mguu wake wa kushoto unaomwezesha pia kupiga mashuti makali. Uwezo wake wa kuwachambua wengine kwenye sehemu ya kiungo umemfanya afananishwe na Patrick Vieira. Ujuzi wake wa kumiliki mpira umewafanya wachambuzi wa soka kumfananisha na Ozil, lakini kazi kubwa inafanywa na mguu wake wa kushoto.
4. John Arne Riise - Fulham
 
Ujuzi wake alianza kuonekana wakati alipokuwa kwenye kikosi cha Liverpool kabla ya kuhamia Fulham. Amekuwa akifunga mabao muhimu kwenye kikosi hicho. Uwezo wake wa mguu wa kushoto umemfanya aimudu vyema nafasi ya beki wa kushoto na winga. Staa huyo wa Norway pia ni fundi wa mipira iliyokufa.
3. Robin van Persie - Man United
 
Kwenye orodha ya washambuliaji wa Ligi Kuu England kama kuna mchezaji ambaye mabeki wanakuwa na hofu pindi mpira unapokuwa kwenye mguu wake wa kushoto basi ni straika wa Kidachi, Robin van Persie.
Fowadi huyo anafahamu namna ya kuutumia mguu wake huo na kufunga mabao ya aina tofauti ikiwamo mipira ya adhabu. Hakika ndiye straika anayetisha zaidi na mguu wake wa kushoto.
Moja ya mabao yake ni lile alilofunga akiwa Arsenal kipindi ilipomenyana na Charlton Athletic, bao ambalo linatajwa kuwa bora zaidi lililowahi kufungwa kwa mguu wa kushoto kwenye Ligi Kuu England.
2. Mesut Ozil - Arsenal
 
Ndiyo yuko katika msimu wa kwanza kwenye Ligi Kuu England, lakini tayari ameonyesha cheche kali kutokana na ujuzi mkubwa wa kucheza soka kwa kutumia mguu wake wa kushoto.
Mguu huo ndiyo uliotengeneza nafasi kadhaa za kufunga kwenye ligi hiyo na kuipa faida kubwa Arsenal msimu huu kwenye Ligi Kuu England na Ligi ya Mabingwa Ulaya. Akiwa amewahi kuwa chini ya Jose Mourinho walipokuwa pamoja Real Madrid, Mreno huyo alikiri kwamba hakuna mchezaji mwenye ujuzi wa kutumia mguu wa kushoto kama alivyo Ozil.
1. Ryan Giggs - Man United
Gwiji lao. Giggs kwa karibu miongo miwili mfululizo amekuwa akiwakimbiza mabeki wa timu pinzani kwa kutumia mguu wake wa kushoto na kuwa mchezaji mwenye hadhi kubwa kwenye Ligi Kuu England. Umahiri wa mguu wake huo umemtambulisha kiungo huyo wa Manchester United kuwa nyota hatari kwa miaka yote 20 aliyodumu kwenye ligi hiyo.
Amefunga mabao zaidi ya 114 kwenye kikosi hicho cha Manchester United, huku bao lake alilofunga dhidi ya Arsenal kwenye Kombe la FA likibaki kuwa kwenye kumbukumbu ya kipekee.

No comments:

- See more at: http://www.helperblogger.com/2012/06/jquery-facebook-like-box-popup-with.html#sthash.AGJhd6Gy.dpuf