Blogger Widgets

Friday, 27 December 2013

Kuondolewa Nchimbi , wenzake ni ajali kazini au...

 
Huenda safari ya kisiasa kama za waziri kwa Dk Emmanuel Nchimbi na wenzake watatu kuwa imekamilika.
Ni baada ya wiki jana Rais Jakaya Kikwete kutengua uteuzi wake pamoja na kina Dk Mathayo David Mathayo (Mifugo na Uvuvi), Balozi Khamis Kagasheki (Maliasili na Utalii) na Shamsi Vuai Nahodha (Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa).
Hata hivyo, Dk Nchimbi amekuwa ni mmoja kati ya viongozi ambao ni vigumu kuwasahau katika uongozi wao kama waziri kwani alionekana mcheshi au mtu mkarimu.
Mbali na hilo pia alikuwa waziri asiyependa kujinadi, hakuwa mwenye hasira mbele ya umma, pengine ilitokana na wizara aliyokabidhiwa.
Aliteuliwa mwaka 2010 akiwa Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo kabla ya kuhamishiwa Mambo ya Ndani ambako Operesheni Tokomeza imemwondoa.
Dk Nchimbi ameondolewa katika nafasi hiyo huenda wako ambao wamepumua au kusherehekea wakati huu wa sikukuu hizi za mwisho wa mwaka. Kwa kipindi cha miaka mitatu aliyokaa katika nafasi hiyo wako ambao wamekiona ‘cha mtema kuni’ huku baadhi yao wakipoteza maisha mikononi mwa polisi, idara ambayo ilikuwa chini yake.
Muda wa miaka mitatu, mwanasiasa huyu binafsi au wizara yake imekutana na changamoto lukuki ambazo ni pamoja na machafuko katika sehemu mbalimbali ya nchi yaliyohusishwa na siasa, dini, sanjari na ajali. Matukio ya uchomaji moto wa makanisa kule Zanzibar katika kipindi cha uongozi wa Dk Nchimbi pale Mambo ya Ndani ni matukio ambayo wengi watamkumbuka nayo.
Tukio la Mei 5, mwaka huu, lile la mlipuko wa bomu uliotokea kwenye Kanisa Katoliki la Mtakatifu Joseph Mfanyakazi, Olasiti mkoani Arusha na kusababisha vifo kwa watu watatu na kujeruhi wengine 67 ni miongoni mwa yale ambayo mwanasiasa huyo ameyaacha nyuma yake.
Mei mwaka huu kule Iringa, vurugu baina ya polisi (FFU) na wafanyabiashara ambako watu 50 walikamatwa kutokana na tukio hilo akiwamo Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa (Chadema) kwa madai ya uchochezi, ni mwendelezo wa visa katika uongozi wake.
Mei 22, mwaka huu, vurugu zilizotokea Mtwara na kusasabisha athari kadhaa, zikiwamo majeruhi na watu kupoteza, uhai na makazi ni kumbukumbu nyingine mbaya kwa mwanasiasa huyu.
Bomu lililorushwa kwenye mkutano wa Chadema mjini Arusha na kusababisha majeruhi 10 na watu wawili kufariki dunia ni doa jingine katika zama hizo za Dk Nchimbi.
Hata hivyo, jambo la kushangaza katika mazungumzo yake na waandishi wa habari kuhusu changamoto hizo, Dk Nchimbi alionyesha mfano wa jirani aliyealikwa kwenye msiba usiomhusu.
Ripoti ya matukio ya mauaji iliyotolewa na Kituo cha Sheria na Haki za binadamu ilibainisha kuwa Watanzania 40 waliuawa lakini wahusika hawakukamatwa au kuwajibishwa.
Kwa hiyo, heshima ya Tanzania kama kisiwa cha amani ilianza kuyeyuka na kuacha madoa.
Kwa hiyo, kuondolewa kwa Nchimbi pale Mambo ya Ndani kwa sasa kunaweza kutafsiriwa kwa mitazamo mbalimbali, ingawa si kuhusishwa na uwezo binafsi wa mwanasiasa huyu kijana.
Kwa ufupi, Dk Nchimbi ameondoka Mambo ya Ndani, tumtakie kila heri ila tufungue ukurasa mpya mwaka 2014 na kumkaribisha mrithi wake.
Namwomba Rais Kikwete wakati tukisubiri waziri atakayevaa kiatu hicho kwamba tunahitaji kiongozi makini, mwenye uwezo mkubwa katika kudhibiti mbinu zote zikiwamo uhalifu.
Kikubwa ni kusaidiwa na Jeshi la Polisi lenye viongozi waadilifu, wanaotimiza wajibu wao ipasavyo.
Ninaamini Rais Kikwete atasikia kilio cha Watanzania, hatasita kuwang’oa mawaziri wengine wasio na uadilifu na uwezo wa kutekeleza majukumu yao ipasavyo.

No comments:

- See more at: http://www.helperblogger.com/2012/06/jquery-facebook-like-box-popup-with.html#sthash.AGJhd6Gy.dpuf