
Afya za maelfu ya walaji wa nyama katika Jiji la Dar es Salaam zipo hatarini baada ya kubainika kuwa nyama inayochinjwa katika machinjio mengi haifai kwa matumizi ya binadamu.
Hali hiyo inatokana na mifugo kuchinjwa bila
kufuata taratibu za afya na kuingizwa sokoni, ikiwamo nyama hizo
kutokaguliwa na wataalamu wa mifugo kabla ya kuchinjwa.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili katika
machinjio mbalimbali ya maeneo ya Vingunguti, Ukonga, Kimara Suka,
Tegeta na Mbagala, umebaini taratibu za kuchinja hazifuatwi huku maeneo
hayo yakiwa yamejaa uchafu.
Mwandishi wa habari hizi alifika katika machinjio
hayo kwa nyakati tofauti alfajiri na kushuhudia ukiukwaji wa taratibu za
uchinjaji, ambapo nyama zinatupwa ovyo, kwenye mazingira hatari, huku
nyingine zikiwekwa karibu na madimbwi ya maji machafu.
TMB: Machinjio hayafai
Alipotafutwa kuzungumzia hali hiyo, Msajili wa
Bodi ya Nyama Tanzania (TMB), Suzana Kiango alisema kuwa machinjio yote
yaliyopo jijini Dar es Salaam hayafai.
Kiango alisema kuwa endapo kila mmoja aliye na
jukumu la kusimamia sheria na kanuni za uchinjaji nyama akizitekeleza,
basi machinjio yote ya jijini Dar es Salaam yanastahili kufungwa. Suzana
alisema kuwa Sheria ya Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) namba 1 ya
mwaka 2003 na Sheria ya Magonjwa ya Mifugo Namba 17 ya mwaka 2003 na
kanuni zake za mwaka 2007 zote kwa pamoja hazisimamiwi ipasavyo.
Anataja baadhi ya sifa ambazo machinjio yanatakiwa
kuwa nazo ni mabomba ya kutoa maji safi na salama, maabara ndogo,
mifereji ya kutolea maji machafu, mabanda ya kutunza mifugo kabla ya
kuchinjwa na chumba cha kuhifadhia nyama kabla ya mkaguzi kuifanyia
uchunguzi.
“Hayo ni baadhi tu, yote hayo hayazingatiwi na TMB
tunasema kwamba iwapo sheria na kanuni zitafuatwa, hakika machinjio
yote ya Dar es Salaam yatafungwa,” anasema Suzana na kuongeza:
“Mifugo inapochinjwa inashauriwa iwe imepoteza
fahamu kabla ya kukatwa shingo ili kuwezesha damu kutoka yote katika
misuli, lakini haya hayazingatiwi na uchinjaji unafanyika chini, kila
kitu kinafanyika chini, jambo ambalo ni kinyume na kanuni za uchinjaji.”
Kauli za Wataalamu
Mkaguzi wa nyama ambaye aliomba jina lake
lisiandikwe gazetini alisema kuwa, asilimia kubwa ya nyama inayoliwa na
wakazi wa Jiji la Dar es Salaam siyo salama kiafya kutokana na uchinjaji
wake kutofuata taratibu zinazokubaliwa
Takwimu zinaonyesha kuwa, katika machinjio ya Vingunguti na
Ukonga, ng’ombe kati ya 250 hadi 300 huchinjwa kila siku, huku yale ya
Kimara Suka, Tegeta na Mbagala yakichinja ng’ombe 100 hadi 120 kwa siku.
“Sisi tunapima ng’ombe au mbuzi kabla na baada ya
kuchinjwa, lakini mazingira ya kuchinjia ndiyo tatizo, kwa kweli
hayaridhishi kabisa,” alisema.
Alifafanua kuwa, endapo masharti ya kiafya ya
uchinjaji wa mifugo na ubebaji wa nyama kutoka sehemu moja mpaka
nyingine vingezingatiwa, nyama inayochinjwa Dar es Salaam isingekuwa na
sifa ya kwenda kwa walaji.
“Wanapotaka kuchinja wanamwangusha ng’ombe au
mbuzi chini kitendo ambacho kitaalamu haitakiwi, lakini hata hao
wanaochinja, baadhi bado hawajapima afya zao. Yote haya ni hatari kwa
usalama wa maisha yetu kwa pamoja,” alisema.
Mtaalamu wa mifugo kutoka Halmashauri ya Wilaya ya
Kisarawe mkoani Pwani, Aron Urassa, alisema endapo ng’ombe atachinjwa
kwa kutofuata taratibu anaweza kusababisha vifo kwa watakaokula.
Anaeleza kuwa mazingira ya kuchinjia yanatakiwa
kuwa safi na salama kwa kuwa yapo baadhi ya magonjwa kama kimeta, ambayo
yanaweza kuangamiza maisha ya maelfu ya watu.
Akifafanua zaidi alisema ili ng’ombe aweze
kufanyiwa vipimo sahihi ni lazima awepo eneo la machinjio kwa saa tano
au sita kabla ya kuchinjwa na siyo vinginevyo.
Mizoga huchinjwa
Mmoja wa wafanyakazi katika machinjio ya Kimara
Suka wilayani Kinondoni aliyejitambulisha kwa jina la Dogo Mwilo,
alilidokeza gazeti hili kuwa baadhi ya ng’ombe huchinjwa na kuuzwa
kinyemela wakiwa tayari wamekufa (mizoga) kutokana na kusafirishwa
umbali mrefu.
“Mwanangu unakuta masela wanawachukua hao ng’ombe,
wanawaichinja na kwenda kuuza nyama. Sasa sijui huwa wanakwenda
kuziuzia wapi, lakini maofisa afya wanakuwa hawajui, si unajua tena
‘life’ (maisha) ngumu,” alisema Dogo Mwilo.
Kwa upande wake, mmoja wa wafanyabiashara wa
ng’ombe kutoka Arusha alisema: “Huwezi kusafirisha ng’ombe zaidi ya 50
halafu wakafa watano, utawatupa wote? Hiyo ni ngumu.”
Alibainisha kuwa licha ya kuwapo wakaguzi, lakini
hakuna linaloshindikana kwani njia za mkato hutumika kuhakikisha ngombe
hao wanachinjwa na kuingizwa sokoni.
“Wewe ndugu yangu, kweli ng’ombe watano wote uwatupe? Hiyo
itakuwa hasara kubwa. Sisi tunajua tunavyofanya hadi kuhakikisha
wanachinjwa pasipo watu kujua, lakini ni makosa kutokana na imani za
dini kupingana na hilo.
Hali ilivyo machinjioni
Ukifika kwenye machinjio yote ya Dar es Salaam,
utapokewa na harufu mbaya na kali, huku mifereji mingi ya kupitisha maji
taka ikiwa imeziba na damu kusambaa eneo kubwa la machinjio husika.
Uoshaji wa utumbo ndiyo kero zaidi, kwani wengi
huoshea kwenye sakafu isiyo safi huku pia maji yanayotumika yakiwa siyo
salama. Kwa upande mwingine maini yalionekana yamewekwa sehemu chafu na
mafuta ya ng’ombe kuanikwa juani kama nafaka.
Ofisa Mfawidhi wa Machinjio ya Vingunguti, Juma
Nghanyanga alisema kuwa, biashara ndani ya machinjio ni jambo
linalosababisha hali ya uchafu kuendelea kuwapo na udhibiti wake ni
mgumu.
Alisema kuwa hairuhusiwi kuwa na soko ndani ya
machinjio, kwa kuwa sehemu hiyo ni maalumu kwa kuchinjia mifugo na
kuipeleka nyama sokoni kwa ajili ya kuuzwa. Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa
ya Ilala, Dk Severin Assenga alisema kuwa wanajipanga kuhakikisha
wanakuwa na maduka 10 yenye hadhi ya kuuzia nyama nje ya machinjio hayo
ya Vingunguti.
“Katika mwaka huu wa fedha tumetenga fedha kwa
ajili ya kujenga maduka 10 yatakayokuwa na hadhi ya kuuzia nyama ili
kukabiliana na hali ya usafi wa mazingira ndani ya machinjio hayo,”
alisema Dk Assenga.
Wakataji, wanunuzi wanena
Benedict Julius anayejishughulisha na ukataji wa
nyama katika machinjio ya Ukonga alisema: “Hali ya usafi ni mbaya na
kinachohitajika ni Serikali kujenga machinjio ya kisasa ili kuepuka adha
hiyo.”
Naye Sokoine John aliye katika machinjio ya
Vingunguti alibainisha bei ya huduma akisema kukata bega moja la ng’ombe
ni Sh1,000 na mbavu Sh1,500, lakini akasema kuwa sehemu inayotumika
kuikatakata nyama hiyo ni mbaya.
Mmoja wa wanunuzi wa nyama Abdallah Hussein
alisema, hali ya mazingira katika machinjio yote inatisha na Serikali
inatakiwa kuliangalia suala hilo kwa jicho la karibu.
Alisema kuwa Serikali inaweza kujenga hospitali nyingi na za kutosha, lakini kama vyanzo vya magonjwa haviangaliwi ni kazi bure.
Kwa upande wake, Ofisa Mifugo Mkuu wa TMB, Jeremiah Temu alisema
kuwa mabadiliko makubwa yanahitajika ya uchinjaji ili kuvutia
wafanyabiashara wakubwa wa nyama kununua nyama zinazochinjwa nchini.
“Utakuta Supermarket na hoteli zinaagiza nyama
kutoka nje, yote haya ni kwa kuwa bado sisi tunachinja nyama chini ya
viwango,” alisema Temu.
Alisema kuwa kwa Tanzania ni machinjio manne pekee
yaliyo bora akiyataja ya mkoani Dodoma, Arusha na Sumbawanga mkoani
Rukwa, akisema hayo yana hadhi ya kimataifa na kushauri ng’ombe
wachinjwe huko na kuletwa Dar es Salaam.
Sifa za duka bora
Sheria ya Chakula, Dawa na Vipodozi Namba namba 1
ya mwaka 2003 ya Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) inaelekeza
wafanyabiashara wote kuwa na maduka yaliyojengwa kwa kuzingatia matakwa
ya sheria hiyo.
Baadhi ya sifa hizo ni wafanyakazi kuwa wamepimwa
afya zao na kuvaa nguo za kujikinga jozi mbili nyeupe zilizo safi muda
wote, kuwepo kwa vifaa vya kukatia nyama kama meza, kibao maalumu,
mapanga, visu na misumeno ya umeme, badala ya magogo na kuwe na ndoano
zisizopata kutu za kuning’iniza nyama.
Kauli za majirani
Mkazi wa Ukonga, Bakadi Juma alisema kuwa hali ya uchafu katika machinjio hayo wameizoea kwani imekuwapo kwa kipindi kirefu.
Jirani wa machinjio ya Vingunguti, Frank Thobias
alisema hali ni mbaya kwani harufu ni kali lakini hawajui wafanye nini.
Alisema kuwa Serikali inatakiwa kuliangalia suala hilo kwa umakini zaidi
kwani wanaoathirika ni wananchi wake, akishauri waboreshe machinjio au
kuyahamisha na kuyapeleka nje ya jiji.
Kauli ya Serikali
Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Dk David
Mathayo alisema kuwa, mpango wa Serikali ni kujenga machinjio ya kisasa
Ruvu mkoani Pwani.
Kuhusu machinjio ya Vingunguti, alisema kuwa Manispaa ya Ilala ndiyo yenye jukumu la kuisimamia na siyo Serikaki Kuu.
Mkakati upo na mchakato wa kumpata mkandarasi atakayejenga machinjio hayo Ruvu unaendelea, ndani ya miaka miwili au mitatu utakuwa umekamilika,” alisema Dk Mathayo
Mkakati upo na mchakato wa kumpata mkandarasi atakayejenga machinjio hayo Ruvu unaendelea, ndani ya miaka miwili au mitatu utakuwa umekamilika,” alisema Dk Mathayo
No comments:
Post a Comment