Blogger Widgets

Thursday, 14 November 2013

Kupigana nondo,kuzika watu wakiwa Hai,kuchuna ngozi, vurugu zinavyouchafua Mkoa wa Mbeya

 
Imani hizo zimesababisha watu watano kuzikwa wakiwa hai, masoko kuungua, watu kuchunwa ngozi na kujeruhiwa kwa nondo.
Siri ya migogoro na matatizo ya vurugu mkoani Mbeya yakiwamo ya kuungua kwa masoko imefichuka, baada ya machifu kupitia Taasisi ya Muungano wa Jamii Tanzania (Mujata) kugundua kuwa ni ushirikina uliokithiri wa wafanyabiashara. Machifu wanasema vitendo hivyo kwa kiasi kikubwa vinachangia kuvuruga kasi ya maendeleo ya mkoa huo.
Kwa mujibu wa Mujata, hata viongozi nao hasa wale wa kisiasa wanachangia kuwepo kwa hali tete mkoani humo, kwa kushindwa kuwapa taarifa wananchi, huku wengine wakijiingiza katika ufisadi kupitia wananchi.
Masoko kuungua mara kwa mara
Mwenyekiti wa Mujata nchini, Chifu Shayo Masoko anasema chanzo cha masoko kuungua mkoani humo, ni kuwepo kwa imani za kishirikina miongoni mwa wafanyabiashara wanaolezwa na waganga kuwa wakichoma moto mali zao na za wenzao watapata utajiri zaidi.
Taarifa zilizopo tayari masoko manne mkoani humo yameshaungua moto, japo vyanzo vyake havikuwa vikihusishwa na imani za kishirikina. Kwa mfano, mwaka 2006 Soko Kuu la Mkoa wa Mbeya  la Mwanjelwa liliteketea kwa moto katika mazingira ya kutatanisha na kuwafanya wafanyabiashara karibu 800 kuhamishiwa kwenye eneo la Sido ambapo walijenga vibanda vya soko jipya, lakini likaungua tena baada ya mwaka mmoja.
Mwaka 2009 Soko la Tunduma liliko mpakani mwa Tanzania na Zambia liliungua na baadaye mwaka 2010 soko kongwe la  Uhindini jijini hapa liliteketea kwa moto  katika mazingira ya kutatanisha.
Hata hivyo, Katibu Tawala wa Mkoa wa Mbeya, Mariam Mtunguja anasema Serikali inaamini kwamba masoko ya Mwanjelwa na Uhindini yaliungua kutokana na  hitilafu ya umeme, wakati lile la Sido liliungua kwa moto wa mama lishe.
Kwa upande wa Mujata,  Chifu Masoko anasema kutokana na kukithiri kwa  matukio hayo, viongozi wa taasisi yake walikutana na kupokea taarifa za  walinzi wa kijadi,   waliotoa taarifa kwamba siri ya kuungua kwa masoko hayo ni ushirikina uliokithiri.
Walisema kuwa baadhi ya wafanyabiashara waliahidiwa kupata mtaji mkubwa kama wangeunguza moto bidhaa zao na za wafanyabiashara wengine.
’Katika uchunguzi wa kimila tulibaini kwamba mpango huo ulitaka kufika kwenye masoko ya Mbalizi na Wilaya ya Momba, jambo ambalo tulilazimika kufanya mikutano ya hadhara kukemea waziwazi tabia hiyo ya ushirikina’’ anasema.
Mitaa  na sifa za kutisha

Kauli ya Mujata inashabihiana na mtazamo wa watu zaidi ya 10 wa jijini hapa waliohojiwa kuhusu sababu za Jiji la Mbeya kuwa tishio kwa vituko.
Watu hao ambao majina yao yanahifadhiwa wanasema Mykoa wa Mbeya una maeneo yanayojulikana kwa sifa mbalimbali mbaya na vituko vya aina yake.
‘’ Karibu Mbeya, lakini ujue wazi kwamba maeneo ya Soko Matola na Block T ni ya wajane, eneo la Mbalizi ni maarufu kwa wizi wa mafuta ya dizeli, Uyole ni maarufu kwa kufungua pipe (mabomba) za magari yaanguke ili waibe bidhaa. Tunduma ni maarufu kwa utajiri wa ushirikina na  Mbozi ni maarufu kwa kuua na kuchuna ngozi’’, anasema mkazi mmoja.
Maeneo mengine anayotaja ni Mwanjelwa ambalo ni maarufu kwa wizi wa mifukoni, Airpot mjini kwa wafadhili wa kupiga nondo, Soweto la matapeli na watengenezaji wa noti bandia, Block Q  la wafadhili wa ujambazi wa silaha, wakati mitaa ya  Isanga ni maarufu kwa uchawi.
Watu kuzikwa hai
Haya nayo siyo matukio mageni mkoani Mbeya na kwa hakika yamekuwa yakiuchafua mkoa huo.
 “Mkoa huu ulishachafuliwa kwani  ilizuka hata tabia ya kuzika watu wakiwa hai kwa tuhuma za ushirikina. Maeneo ambayo watu walizikwa wakiwa hai ni kijiji cha Maramba wilayani Mbarali,  Isyesye  nje kidogo ya Jiji la Mbeya, Mkwajuni Chunya na huko wilayani Momba’’ anasema Chifu Masoko na kuongeza kuwa tukio kama hilo limejitokeza tena kwenye kijiji cha Mshewe kilichopo  Mbeya Vijijini.
 Anasema kwa kushirikiana na Serikali, Mujata imezunguka katika vijiji na miji mbalimbali kutoa elimu na kukemea tabia hiyo,  ikiwa ni pamoja na kusuluhisha migogoro ya kifamilia, ardhi  na hata migogoro ya kisiasa na kiuchumi.
‘’Ushirikina mwingine wa wafanyabiashara unahusisha kuua watoto, kuwaua wazazi huku wengine wakidaiwa kufuga misukule’’, anaeleza  na kusisitiza kwamba Mujata itaendelea kukemea vitendo hivyo.
Viongozi lawamani
Kuhusu kauli za baadhi ya viongozi kwamba wakazi wa Mkoa wa Mbeya  wana tabia ya ubishi na kutaka wajitawale, Chifu Masoko anaipinga na kusema tatizo lililopo ni wananchi kutoshirikishwa katika uamuzi wa mambo yanayowahusu.
 ‘’ Kwa mfano, wakulima na wafanyabiashara wa ndizi Rungwe waligoma kwa sababu  baada ya madiwani kupokea taarifa ya kutaka kupandisha ushuru  kwa asilimia 100 hawakurudi kwa wananchi kuwaeleza ili kupata maoni’’ anasema na kuongeza:
‘’Pia wakala wa kukusanya ushuru alipatikana kwa utata, kwani  wananchi walimhusisha na kiongozi mmoja aliyemleta wakala huyo kwa njia za utata kutoka mkoani kwake.’’
Aidha, Chifu Masoko anadokeza pia kwamba mfumo wa vyama vingi umechangia kuharibu maadili ya vijana, huku baadhi ya viongozi wa kisiasa nao wakiwashawishi wananchi kuwapinga viongozi waliochaguliwa kwa njia halali.

No comments:

- See more at: http://www.helperblogger.com/2012/06/jquery-facebook-like-box-popup-with.html#sthash.AGJhd6Gy.dpuf