Blogger Widgets

Wednesday, 6 November 2013

Eriksson: Nilisaini Kuifundisha Man United

 
KOCHA Sven-Goran Eriksson amedai kwamba alishasaini mkataba wa kuinoa Manchester United kurithi mikoba ya Sir Alex Ferguson mwaka 2002.
Kocha huyo alidai hayo kupitia kitabu chake kwamba mabosi wa Manchester United walimfuata wakati huo akiwa anaionoa England na Ferguson alitanganza kwamba anajiandaa kustaafu.
Kwenye kitabu hicho, Eriksson aliandika: “Nilijua ulikuwa mtego. Nilikuwa na mkataba na England hadi fainali za Kombe la Dunia 2006 na ningeandamwa sana kama ningevunja mkataba.
“Lakini, ilikuwa bahati kupata nafasi ya kuinoa Manchester United. Nilisaini mkataba, hivyo nilikuwa kocha mpya wa timu hiyo.”
Lakini, mwishowe Ferguson aliamua kubaki kwenye klabu hiyo kwa miaka mingine 11 kabla ya kustaafu mwishoni mwa msimu uliopita.
Kwenye kitabu hicho, Eriksson alidai pia kuwahi kulumbana na Ferguson juu ya straika Wayne Rooney kujumuishwa kwenye kikosi cha England kilichocheza fainali hizo za Ujerumani.
“Leif (Sward) daktari wa England na mimi tulikutana na Ferguson na daktari wa Manchester United kwenye uwanja wao wa mazoezi. ‘Hawezi kucheza Kombe la Dunia’, alisema Ferguson. Daktari alileta vipimo vya X-rays na kuonyesha mfupa wa Rooney uliokuwa umevunjika, haukuwa umepona kwa wakati.
“Wakati daktari huyo alipomaliza kueleza, Leif alimtazama usoni na kisha akamwambia ‘Kwanini umeketi hapa na kunidanganya?’ Leif alikuwa mmoja ya wataalamu Ulaya kuhusu majeruhi kama aliyapata Rooney. Natamani ningemrekodi kwenye video sura ya Ferguson ilivyokuwa wakati Leif alipokuwa akielezea kuvunjika kwa Wayne na muda wa kucheza Kombe la Dunia.
“Leif alipomaliza kueleza, nilimgeukia Ferguson, nikamwambia ‘Samahani Alex, nitamchukua Rooney’.”
Rooney alikwenda kwenye fainali hizo, lakini hakufunga bao lolote na kuishia kuonyeshwa kadi nyekundu kwa kumtendea madhambi Ricardo Carvalho.

No comments:

- See more at: http://www.helperblogger.com/2012/06/jquery-facebook-like-box-popup-with.html#sthash.AGJhd6Gy.dpuf