Blogger Widgets

Sunday, 20 October 2013

Mkorogo:Unauzwa kijiko Sh1,000, wamiminika kununua


Licha ya Serikali kupitia mamlaka husika mara kadhaa kuchukua hatua ya kukemea na kukataza matumizi ya vipodozi vyenye kemikali, lakini kadiri siku zinavyozidi kwenda matumizi ya bidhaa hizo yanaonekana kushika kasi katika maeneo mengi nchini.
Ripoti iliyotolewa hivi karibuni na Profesa Msaidizi wa Chuo Kikuu cha Georgia, Marekani, Kelly Lewis wa kitengo cha Sosholojia inaonyesha kuwa asilimia 30 ya wanawake nchini Tanzania ambayo ni sawa na wanawake milioni sita, wanatumia mkorogo wenye mchanganyiko wa vipodozi vyenye kemikali hatari kwa afya ya binadamu.
Uchunguzi uliofanywa  umegundua kuwapo kwa njia mpya za kutengeneza mkorogo (mchanganyiko unaotumika kubadili rangi ya ngozi na kuwa nyeupe), ambao huuzwa kwa bei nafuu huku makundi ya wanawake wakionekana kumiminika katika soko la Tandika kujipatia bidhaa hiyo.
Mikorogo hiyo ya kila aina ambayo hutengenezwa kulingana na matakwa ya muuza vipodozi hujazwa kwenye ndoo zenye ujazo wa lita tano mpaka lita 10 na kupimwa kwa kutumia kijiko cha chakula na kuuzwa kwa bei ya Sh1,000.
Ingawa kila mmoja hutengeneza kutokana na matakwa yake lakini wauzaji wengi wa mkorogo wametaja kuchanganya aina kadhaa za losheni, ambazo mara kadhaa zimetajwa kuwa na kemikali ambazo si nzuri kwa mwili wa binadamu.
Miongoni mwa losheni zinazopatikana katika mchanganyiko huo ni pamoja na Carolite, Princess claire, Bioclaire, Miki, Super Rico, Top lemon, Tenteclaire, Extraclaire, Caronite, Biocarrot na nyinginezo. Kwa mujibu wa wataalamu idadi kubwa ya vipodozi hivi vimepigwa marufuku kutokana na madhara yake kwa afya ya mtumiaji.
Kipimo kinachotumika ndiyo kimeupa jina aina hii mpya ya mkorogo na kujulikana zaidi sokoni hapo kama ‘kijiko’ huku maeneo mengine ya jiji ukifahamika kwa majina mbalimbali kama vile ‘king’amuzi’ na ‘king’asti’.
Mwandishi wa habari hii alishuhudia biashara hii ya kijiko ikifanyika kwa kasi sokoni hapo, huku baadhi ya wauzaji wakiendelea kuwajibika katika utengenezaji ili kuhakikisha watu wanaendelea kujipatia bidhaa hiyo.
Juma Seleman ambaye ni mmoja wa wauzaji na watengenezaji wa mkorogo huo aliweka wazi kuwa aina mbalimbali za losheni zaidi ya 20 hutumika katika kupata mchanganyiko huo, ambao kila mtengenezaji huwa na rangi yake kulingana na vitu anavyotumia.
“Kila mmoja ana losheni zake anazoweka ingawa mimi huwa nachanganya kali na zile zilizopoa ili isimchubue sana mtu, lakini wapo ambao huweka losheni kali tupu hizo huweza kuwa na madhara na kuharibu ngozi,” alisema Seleman.
Seleman aliweka wazi kuwa wauzaji wengi wa vipodozi wamefikia hatua ya kutengeneza mikorogo hiyo ili kuwawezesha watu wa hali ya chini kumudu gharama na ndiyo maana huuzwa kwa bei nafuu.
“Hii inasaidia kumrahisishia mteja badala ya kununua losheni, sabuni na maji yake ambayo gharama yake inaweza kufika Sh10,000 anaweza kupata kitu kizuri kwa bei ya chini ya hapo na ikawa na matokeo mazuri katika ngozi,” alisema Seleman huku akipaka mchanganyiko huo kuonyesha mfano.
Aidha alibainisha kuwa kwa ndoo moja ya lita 10 anaweza kuuza na kupata pesa isiyopungua Sh laki mbili, kulingana na kasi ya mauzo na ndoo huisha kati ya siku moja mpaka tatu.
Mmoja wa wanunuzi wa mkorogo huo aliyejitambulisha anaitwa Mama Hamis, alisifia ubora wake na kudai kuwa umekuwa na matokeo mazuri katika ngozi yake na kuwa mng’ao wenye mvuto.
“Nunua tu dada inakufanya unakuwa mzuri ngozi inakuwa laini na wala hupati madhara yoyote, kwani ingekuwa na madhara basi ningeshaona lakini tangu nimeanza kutumia sijadhurika chochote,” alieleza Mama Hamis.
Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) kupitia msemaji wake, Gaudensia Simwanza, ilikiri kuwapo kwa changamoto ya baadhi ya wafanyabiashara kutengeneza mikorogo hiyo kwa kificho, licha ya mara kwa mara kuwakamata na kuwafikisha katika vyombo vya dola.
Simwanza alibainisha kuwa asilimia kubwa ya vipodozi vinavyotumika kutengeneza ‘kijiko’vimepigwa marufuku kutokana na kuwa na viambato vyenye sumu, ambayo kwa kiasi kikubwa ina madhara katika ngozi na mfumo mzima wa mwili wa binadamu.
“Tumekuwa tukitoa elimu mara kwa mara kwa wananchi kuhusiana na madhara ya matumizi ya vipodozi hivi, na wanapaswa kujua anayewakorogea na kuwachanganyia kemikali hana nia njema na afya zao, waepuke na kutoa taarifa ili wachukuliwe hatua,” alisema Simwanza
Kwa mujibu wa TFDA vipodozi vyenye sumu ni pamoja na top lemon, krimu ya princess na losheni zake, Extra clair, krimu ya viva super lemon, clere lemon, Mekako na nyinginezo ambazo huwa na kiambato cha Hydroguinone ambacho husababisha muwasho wa ngozi, mzio sambamba na kusababisha mabaka mwilini.
Vingine ambavyo vimetajwa kuwa na sumu kali ya Hydroquinone ni Carolight, G&G teint uniforme, G&G Dynamiclair, Bioclare, Maxi white na sabuni za Miki, Jaribu, Rico, Tura, Mekako, Movate na nyinginezo ambazo tayari zilishapigwa marufuku kutokana na kusababisha madhara kadhaa ikiwemo kansa ya ngozi.
Vipodozi vingine ambavyo vinatajwa kuwa hatari kwa afya ya binadamu ni pamoja na vile vilivyotengenezwa kwa kutumia madini ya Zebaki, ambayo husababisha madhara ya ngozi, ubongo, figo na viungo mbalimbali vya mwili.

No comments:

- See more at: http://www.helperblogger.com/2012/06/jquery-facebook-like-box-popup-with.html#sthash.AGJhd6Gy.dpuf