Blogger Widgets

Wednesday, 23 October 2013

Beckham, Van Nistelrooy kukiona kwa Ferguson


KOCHA wa zamani wa Manchester United, Alex Ferguson,  amewaonya wachezaji wa zamani na wa sasa wa klabu hiyo akiwaambia hataficha kitu chochote katika kitabu cha maisha yake kinachotazamiwa kuzinduliwa keshokutwa Alhamisi.
Kitabu cha Ferguson kitaandika matukio aliyoyaona kuanzia mwaka 1999 alipotoa kitabu chake cha kwanza mpaka Mei mwaka huu alipostaafu kuifundisha timu hiyo.
Ferguson ameahidi kufichua siri za sakata linalomzunguka mshambuliaji, Wayne Rooney, pamoja na sakata lililozunguka katika uuzwaji wa mastaa wa zamani, David Beckham na Ruud van Nistelrooy, ambao kwa nyakati tofauti walikwenda Real Madrid.
Wakati inasemekana Beckham aliuzwa kwa sababu ya kubadili mfumo wake wa maisha mara baada ya kumuoa mwanamuziki wa kundi la Spice Girls, Victoria Adams ‘Posh’, Van Nistelrooy inasemekana aliondoka baada ya mzozo wake na Cristiano Ronaldo mazoezini.
“Unajua tatizo la kuandika kitabu ni kwamba inabidi uandike vitu vidogo vidogo ambavyo vinaathiri au kupima uwezo wako wa kufanya maamuzi. Lakini kwa sababu nimekuwa katika klabu hii kwa muda mrefu, nikijenga timu baada ya timu, kuna maeneo ambayo hauwezi kuyapuuza,” alisema.
“Kwa mfano tuliwahi kuwauza wachezaji kama David Beckham na Ruud van Nistelrooy. Hauwezi kupuuza mambo haya kwa sababu hawa walikuwa wachezaji wakubwa, wenye mamlaka makubwa katika historia ya Manchester United.”
Ferguson pia anatarajiwa kueleza jinsi ambavyo Wayne Rooney alitazamiwa kuondoka Old Trafford mwaka 2011 kabla hajasaini mkataba mpya siku chache zilizofuata.
Anatarajiwa pia kueleza tena jinsi Rooney alivyoomba kuhama kwa mara nyingi katika dirisha lililopita, kama ambavyo Ferguson mwenyewe alikaririwa akiwaambia mashabiki waliojazana kuhudhuria pambano kati ya Manchester United na Swansea Mei mwaka huu wakati akiwaaga pale Old Trafford.
Katika kitabu hicho, Ferguson anakiri kwamba kupoteza ubingwa kwenda kwa Manchester City mwaka 2012 ilikuwa moja kati ya pigo kubwa katika maisha yake ya soka Manchester United.
Kocha huyo raia wa Scotland pia anatazamiwa kufichua ugomvi uliojificha na nahodha wake wa zamani, Roy Keane, ambaye awali alikuwa rafiki yake mkubwa, lakini katika siku za karibuni Keane amekuwa akimshambulia Ferguson kwa madai kwamba hakumlinda wakati anaondoka zake Old Trafford.

No comments:

- See more at: http://www.helperblogger.com/2012/06/jquery-facebook-like-box-popup-with.html#sthash.AGJhd6Gy.dpuf