Blogger Widgets

Saturday, 3 August 2013

Chai maharage zamponza Shaaban Kondo wa Yanga

 
STRAIKA mpya wa Yanga, Shaaban Kondo amekaribishwa Jangwani kwa adhabu baada ya kukatwa mshahara wake kwa kosa la kucheza mechi za mchangani maarufu kama ‘chai maharage’.
Kocha Msaidizi wa Yanga Fred Felix Minziro ameithibitishia Mwanaspoti kuwa wamemkata  mchezaji huyo Sh 200,000 kwa kosa hilo huku akimpa onyo jingine kali.
Inadaiwa kuwa mshambuliaji huyo alishindwa kujizuia kufanya tukio hilo jioni ya Jumatatu iliyopita licha ya asubuhi kocha wake kutoa onyo mazoezi kwa wachezaji wake kuacha tabia hiyo ili yasije yakawakuta mabaya.
Habari zinadai zaidi  kuwa Minziro alishtukia dili la baadhi ya wachezaji wake kutakiwa kucheza ndondo sehemu siku hiyo na alifanya makusudi kuwaita wachezaji wake wote baada ya mazoezi  na kuwausia kutofanya jambo hilo kwani ni hatari kwa afya zao endapo wataumia na pia wanaweza kukatwa mishahara yao.
Inadaiwa kuwa Kondo na beki mmoja wa klabu hiyo ndiyo walikuwa wakihusishwa kucheza ndondo siku hiyo lakini cha kushangaza maneno ya kocha wake hayakumuingia vizuri Kondo na kwenda kucheza ndondo jioni huku mwenzake akikataa kufanya hivyo kwa kuogopa adhabu.
“Inashangaza, asubuhi nimetoka kulizungumzia jambo hilo na kila mchezaji alisikia lakini cha kushangaza jioni mchezaji anakwenda kucheza ndondo. Ni jambo baya sana kwani unaweza ukaumia huko, sasa sijui unafanyaje maana unaweza ukakaa nje muda mrefu ikawa ni hasara kwako na hata kwa klabu yako pia,” alisema Minziro.
Aliongeza: “Kweli tumemkata Sh 200,000 kama adhabu ya kosa hilo na tumempa onyo endapo akirudia atapata adhabu nyingine  kubwa zaidi ili kukomesha vitendo kama hivi.
“Tena hii adhabu itaendelea kwa mchezaji yoyote atakeyeonekana amekwenda kucheza mchangani (ndondo). Hii ni klabu kubwa  lazima wachezaji wake pia waishi kiprofesheno,”alisema Minziro.
Hata hivyo Kondo alipoulizwa kuhusiana na jambo hilo aligoma katakata kuelezea na kudai kuwa tuachane na hilo suala. 
Yanga inaendelea na mazoezi kwenye Uwanja wa Bora Kijitonyama na jana Ijumaa walitarajia kurudi kwenye Uwanja wa Shule ya Loyola kujiandaa na Ligi Kuu Bara msimu ujao ambayo itaanza  Agosti 24.
Yanga inanolewa na kocha msaidizi Minziro baada ya kocha mkuu Ernest Brandts kuwa katika kozi ya ukocha nchini Ujerumani na alitarajiwa kurejea nchini jana Ijumaa au leo Jumamosi.

No comments:

- See more at: http://www.helperblogger.com/2012/06/jquery-facebook-like-box-popup-with.html#sthash.AGJhd6Gy.dpuf