Blogger Widgets

Tuesday, 13 August 2013

Bodaboda wamejitangazia Jamhuri?

 
Tumelazimika tena leo kuitahadharisha Serikali na mamlaka mbalimbali zinazosimamia usafiri wa pikipiki, maarufu kama bodaboda kwamba usafiri huo sasa umekuwa janga la kitaifa. Tulitoa tahadhari hiyo mapema mwaka huu, ingawa wakati huo matatizo lukuki na ya kutisha yanayosababishwa na madereva wa vyombo hivyo vya usafiri hivi sasa yalikuwa hayajawa makubwa.
Tulitahadharisha wakati huo kwamba usafiri huo wa bodaboda ulikuwa ukielekea pabaya kwa maana ya kuhatarisha usalama wa abiria, wananchi wanaotembea kwa miguu na madereva wa vyombo vingine vya usafiri barabarani. Tulisema kwamba usafiri wa bodaboda ni jambo la kudumu kutokana na ukweli kwamba tayari umewapatia ajira maelfu kwa maelfu ya vijana ambao wengi wao walikuwa vijiweni wakijihusisha na vitendo vya uhalifu kama ukabaji na uvutaji bangi, hivyo hatua zozote za kuupiga marufuku zingewasukuma vijana hao warudi mitaani na kusababisha sintofahamu.
Sisi tuliishauri Serikali iimarishe Sumatra kwa kuhakikisha inaweka viongozi wachapakazi, wenye uwezo, dira na mwelekeo ili kuudhibiti usafiri huo ambao tayari ulikuwa umekielemea Kikosi cha Usalama Barabarani. Tulishauri uwekwe utaratibu wa kuwafundisha madereva wa vyombo hivyo sheria za barabarani ili kupunguza idadi ya vifo vilivyokuwa vikitokea kila kukicha kutokana na ajali za barabarani.
Inasikitisha kuona kwamba sasa tatizo hilo limepanuka maradufu na Serikali na taasisi zake husika havionyeshi dhamira ya kupata suluhisho la hali hiyo. Sumatra ambayo ndio yenye dhima ya kudhibiti vyombo vya usafiri imekuwa dhaifu mno kiasi cha kushindwa angalao kuhakikisha kwamba usafiri wa bodaboda unakuwa ni salama na madereva wa vyombo hivyo wanafahamu na kuheshimu sheria za barabarani.
Takwimu za hivi karibuni zinaonyesha kuwa, katika Jiji la Dar es Salaam pekee, wastani wa madereva watatu wa bodaboda hufariki kwa ajali kila siku. Madaktari na wauguzi katika Kitengo cha Mifupa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili wamesema wameelemewa na kazi ya kuwahudumia majeruhi wa ajali za bodaboda kutokana na idadi yao kuongezeka siku hadi siku.
Imethibitika kwamba sio tu usafiri huo sasa umekuwa janga la kitaifa, bali pia kwamba ajali nyingi zinazosababisha vifo na ulemavu wa viungo zinasababishwa na madereva wa bodaboda. Usafiri huo umekosa udhibiti na kusababisha madereva wake kufanya watakalo. Madereva wengi wanakwenda mwendo wa kasi ya ajabu na ni chanzo cha vurugu kila mwenzao anapopata au hata anaposababisha ajali. Tunaambiwa vijana hao wameunda “jeshi”, hivyo wanajichukulia sheria mkononi kwa kupiga watu kwa kutumia mapanga, visu na nondo. Wengi wamethibitika kupata ajali wakiwa wametumia dawa za kulevya au wakiwa wametumia pombe kali.
Waendesha bodaboda wengi ni hatari hivi sasa. Wamejiingiza katika uhalifu wa mauaji, wizi na uporaji. Matukio makubwa ya uhalifu kama ya kumwagia watu tindikali, mauaji na kadhalika sasa yanafanywa kwa kutumia bodaboda. Kama tulivyosema hapo juu, mamlaka za udhibiti husika ziko likizo au zimelala usingizi wa pono.
Madereva hao wanadaiwa kujiundia ‘Jamhuri’ kutokana na kujiona kuwa juu ya sheria. Askari wa Barabarani wanaogopa kuwagusa na hakuna anayehakikisha wanapata vitambulisho maalumu, usajili wa uhakika na uratibu wa karibu wa biashara hiyo, ikiwa ni pamoja na bodaboda hizo kupewa namba maalumu na kupakwa rangi kufuatana na manispaa au wilaya zilikosajiliwa.

No comments:

- See more at: http://www.helperblogger.com/2012/06/jquery-facebook-like-box-popup-with.html#sthash.AGJhd6Gy.dpuf