Blogger Widgets

Wednesday, 27 November 2013

Zaidi ya taasisi 120 za elimu ya juu na utafiti zinafungwa vifaa vya mtandao vitakavyoviunganisha na Mkongo wa Taifa


Ili kuziwezesha kupata rejea za masomo na kuingia kwenye mfumo wa taarifa za kitaaluma.
Dar es Salaam. Zaidi ya taasisi 120 za elimu ya juu na utafiti zinafungwa vifaa vya mtandao vitakavyoviunganisha na Mkongo wa Taifa  ili kuziwezesha kupata rejea za masomo wanayochukua, mawasiliano na kuingia kwenye mfumo wa taarifa za kitaaluma za ndani na nje ya nchi.
Hayo yalisemwa mwishoni mwa wiki na Naibu Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na  Teknolojia, Januari Makamba wakati akipokea vifaa vya mradi wa Sayansi Teknolojia na Elimu ya Juu vitakavyofungwa awamu ya kwanza katika taasisi 28 kwa kuziunganisha kwenye Mkongo wa Taifa.
Makamba alisema mradi huo unafadhiliwa na Benki ya Dunia iliyoikopesha Serikali Dola 100 milioni kwa ajili ya kuutekeleza. Mkandarasi M/S Softnet Technologies Ltd Tazania ndiye aliyepewa kazi ya kufunga vifaa hivyo.
“Katika kipindi cha Desemba na Februari mwakani vifaa vyenye thamani ya Dola 2.2 milioni vitakuwa tayari vimefungwa katika taasisi 28 na kuanza kutumika,” alisema Makamba.
Awamu ya kwanza vyuo vya elimu ya juu vitakavyounganishwa ni kutoka Mikoa ya Dar es Salaam, Iringa, Arusha  Mbeya, Kilimanjaro, Morogoro na Zanzibar, likiwamo Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA).
Lengo ni kusaidia kuondoa gharama za mawasiliano vyuoni, kukabiliana na changamoto ya wahadhiri kwa kuwa mhadhiri mmoja atafundisha vyuo zaidi ya 20 kwa kutumia vifaa hivyo vya sayansi na teknolojia na rejea zote zitakuwemo ndani ya maktaba ya mtandao huo za ndani na nje ya nchi, chuo kimoja kitawasiliana na kingine bure bila ya kuwepo gharama.
“Elimu ya juu inategemea kupata manufaa toka maktaba, mradi huu utawawezesha wanafunzi kupata vitabu na taarifa kutoka chuo chochote duniani. Lakini natoa wito kwa wanafunzi na wanaoongoza taasisi za elimu nchini kuvithamini na kuvitunza na kuvitumia kwa manufaa mengine.”

No comments:

- See more at: http://www.helperblogger.com/2012/06/jquery-facebook-like-box-popup-with.html#sthash.AGJhd6Gy.dpuf