
Rais Jakaya Kikwete na Mama Salma Kikwete wakikagua chai ikichambuliwa katika Kiwanda cha Chai cha Ikanga, Njombe, ikiwa ni sehemu ya sherehe za uzinduzi wa Mkoa mpya wa Njombe, Ijumaa iliyopita
Wananchi wa Kijiji cha Makoga Wilaya ya Wanging’ombe mkoani Njombe jana walisimamisha msafara wa Rais Jakaya Kikwete na kumweleza kero zao mbalimbali ikiwamo ya kutaka gari la kubebea wagonjwa (ambulance) kwa ajili ya zahanati ya kijiji hicho.
Wananchi hao walifurika saa nne asubuhi kandokando ya barabara na kuomba msafara wa Rais Kikwete usimame.
Msafara wa Rais Kikwete ulikuwa unatokea Makete
kuelekea Njombe na ndiyo ukakutana na wananchi hao waliokuwa na shauku
ya kueleza matatizo hayo kwa Rais.
Rais Kikwete alikubali kushuka na ndipo baadhi ya
wananchi mmoja mmoja wakaanza kutaja kero zinazowakabili katika Kijiji
cha Makoga.
Wananchi waliomba kuboreshwa kwa huduma ya maji pamoja na kuwahishiwa pembejeo za kilimo.
“Mheshimiwa Rais pia tunaomba gari la wagonjwa
kwani tunapata shida sana kuwapeleka wagonjwa wetu hospitali,” alisikika
mmoja wa wananchi hao akisema.
Majibu ya Rais Kikwete
Akijibu kero hizo za wananchi, Rais Kikwete
aliwaahidi kuwa Serikali yake itatafuta fedha kwa ajili ya kuwaletea
gari la wagonjwa.
Kuhusu pembejeo za kilimo, alisema Serikali
itaangalia uwezekano wa kuongeza pembejeo za kilimo mwakani. Kuhusu maji
alisema kijiji hicho kipo kwenye mpango wa vijiji 10 vitakavyopatiwa
huduma ya maji katika Halmashauri ya Wilaya ya Wanging’ombe katika
bajeti ya mwaka 2013/14.
Pia Naibu Waziri wa Nishati na Madini, George Simbachawene alisema kijiji kipo kwenye mpango wa kuletewa umeme hivi karibuni.
Ahimiza tohara
Pia Rais Kikwete aliwataka wanaume nchini
kuendelea kujitokeza kwa wingi kupata tohara kama moja ya njia za
kukabiliana na ugonjwa wa Ukimwi.
Akisalimia wananchi katika Kijiji cha Kipengele kilichoko katika
Wilaya ya Wanging’ombe, Mkoa wa Njombe, ambako anaendelea na ziara yake
kukagua na kuzindua miradi ya maendeleo, Rais pia amewapongeza wanaume
ambao mpaka sasa wamejitokeza kupata tohara ili kukabiliana na ugonjwa
huo.
Katika hatua nyingine, Rais Kikwete alizindua Chuo
cha Ufundi Stadi (Veta) katika Wilaya ya Makete ikiwa ni chuo cha
kwanza katika mpango wa Serikali wa kuhakikisha kila wilaya inakuwa na
chuo cha ufundi stadi ili kuhakikisha vijana wanapata fursa kujifunza
ujuzi mbalimbali.
Akisoma taarifa ya ujenzi wa chuo hicho,
Mkurugenzi Mkuu wa Veta, Zebedayo Mushi alisema chuo hicho kimejengwa
kwa ushirikiano kati ya Veta na Halmashauri ya Wilaya ya Makete
No comments:
Post a Comment