Blogger Widgets

Monday, 28 October 2013

LIVERPOOL WANGEKOSEA SANA KAMA WANGEMUUZA SUAREZ


MMILIKI wa Liverpool, John W Henry, alitazama mbali. Utakumbuka tu, wakati alipoingia kwenye ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Twitter na kuandika kitu kuhusu straika wa timu hiyo, Luis Suarez.
Ilikuwa Julai 24, yaani miezi mitatu iliyopita ndipo alipotuma maneno yake kwenye mtandao huo. Kilichomsukuma kutuma maneno hayo ni kitendo cha Arsenal kupeleka ofa ya Pauni 40,000,001 ikimtaka straika huyo raia wa Uruguay.
Dhihaka ya Arsenal ndiyo iliyomfanya mmiliki huyo wa Kimarekani kuingia kwenye mtandao. Arsenal iliposikia kwamba Suarez atakuwa tayari kuruhusiwa kuzungumza na klabu yoyote inayomtaka kama itatolewa ofa inayozidi Pauni 40 milioni, basi yenyewe ikaongeza pauni moja tu na kuwa 40,000,001 ili wamnase staa huyo.
Hicho ndicho kilichomfanya Henry kwenda kwenye ukurasa wake wa Twitter na kuwakejeli Arsenal alipoandika: “Hivi ni kitu gani unafikiria watakuwa wanavuta pale Emirates?”
Juzi Jumamosi, aliingia tena kwenye Twitter na kuandika tena kitu kinachohusu Suarez. Safari hii aliandika maneno mawili tu. “Luis. Mchawi.” Ni ngumu kumgomea.
Kwa hali iliyojitokeza kwenye mchezo wao wa juzi Jumamosi dhidi ya West Brom, hauwezi kumkatalia Henry. Suarez alikuwa akikimbia uwanjani Anfield akiwa na tabasamu pana, alifunga mabao kama alivyotaka na kuzima vuruguvugu lote la kutaka kuondoka kwenye usajili uliopita.
Akafunga ‘Hat-Trick’ yake ya kwanza kwenye Uwanja wa Anfield, wakati Liverpool iliposhinda mabao 4-1. Suarez angeweza hata kufunga mabao matano.
Wakati alipokuwa akitoka uwanjani, ikiwa imebaki dakika moja tu mchezo kumalizika alipofanyiwa mabadiliko, aligeuka pande zote nne za uwanja na kuwashukuru mashabiki kwa kumpa sapoti.
Mashabiki wa Liverpool hawakuwa wameliondoa penzi lao kwa straika huyo, lakini kitendo hicho kimezidi kuwarudisha kwenye himaya yake watu wanaomsapoti.
Kwa maana hiyo, Suarez bado yupo sana Anfield licha ya Arsenal kumnyemelea, lakini shukrani kubwa kwake Henry, ambaye hakutaka kabisa kusikia suala kumuuza staa huyo.
Labda angekubali kumuuza kama kungekuja ofa ya nguvu na angefanya hivyo kwa klabu inayotoka nje ya England.
Henry alifahamu wazi kumuuza Suarez ni kuishushia hadhi Liverpool na hakutaka klabu yake ionekane dhaifu kwa kushindwa kugomea klabu nyingine zinapojaribu kuwavamia na kutaka mchezaji kwao.
Kwenye Uwanja wa Anfield juzi Jumamosi, Suarez alionyesha kwa nini Henry alipambana kuhakikisha anabaki. Staa huyo tangu alipoingia uwanjani kupasha misuli akiwa na straika Daniel Sturridge, alionyesha wazi kwamba kuna kitu anataka kukifanya kwa ajili ya mashabiki wake.
Kabla hata hajatumbukiza mipira wavuni, alikuwa akiwakimbiza na kuwasumbua mabeki wa West Brom muda wote na hivyo kumchoka kumzuia. Suarez alicheza kwenye ubora wake.
Imani ya Liverpool imezaa matunda, kwa sababu pamoja na Suarez kuwatikisa kwenye kipindi cha usajili akitaka kuondoka, uamuzi wao wa kumbakiza haukuwa na shaka kwamba angecheza chini ya kiwango kwa sababu wanafahamu hilo si asili yake.
Wanaokwenda kumtazama mazoezini, wale wanaokuwa karibu naye kwenye kikosi, wanamfahamu staa huyo alivyo na moyo wa kupambana muda wote na kiu yake ni kufikia mambo makubwa kwenye soka. Mazoezi anayoyafanya kama ni mchezaji kinda anayetafuta namna ya kutaka kutambulika.
Dhidi ya West Brom alikuwa anafunga huku akitabasamu na hilo linadhihirisha kwamba anachokifanya kinatoka moyoni na anacheza mpira kwa mapenzi yake.
Kwa mujibu wa Suarez sababu moja inayotaka kumwondoa Liverpool ni kushindwa kucheza Ligi ya Mabingwa Ulaya, lakini kwa kiwango cha timu hiyo kwa msimu huu imani ni kubwa kwamba msimu ujao wanaweza kuwamo kwenye michuano hiyo. Ni jambo la kusubiri.
Ni jambo linaloeleweka, wachezaji wote makini wanahitaji kucheza kwenye michuano yenye hadhi kubwa. Kocha Brendan Rodgers anaonekana kuzichanga vyema karata zake na msimu ujao Liverpool inaweza kuzungumziwa kwenye mikikimikiki ya Ulaya.
Lakini, kabla ya kulifikia hilo, shukrani kubwa ni kwa Henry aliyepambana kumbakiza Suarez Anfield na sasa mchezaji huyo anatema cheche.

No comments:

- See more at: http://www.helperblogger.com/2012/06/jquery-facebook-like-box-popup-with.html#sthash.AGJhd6Gy.dpuf