Blogger Widgets

Sunday, 27 October 2013

Tazama unga hatari unavyouzwa kiholela mitaani

 
Afya za Watanzania zipo hatarini kutokana na kula unga ulioandaliwa bila kuzingatia kanuni za afya na kwenye maeneo machafu.
Unga huo ambao umesambaa madukani huandaliwa kwenye mashine ndogo za kusaga, zilizopo katika mitaa ya miji mikubwa nchini.
Bidhaa nyingine za nafaka ambazo zinauzwa na wafanyabiashara hao mitaani bila ya kufuata kanuni za afya ni unga wa ngano, ulezi, mtama, muhogo na uwele.
Uchunguzi wa gazeti hili unaonyesha kuwa wafanyabiashara wadogo wamekuwa wakianzisha miradi ya kusaga mahindi na unga wake kuwekwa katika vifungashio, bila ya kufuata taratibu za afya zilizowekwa na Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) na Shirika la Viwango Tanzania (TBS).
Kwa mujibu wa ripoti ya miaka 10 ya utendaji kazi wa TFDA, kifungu namba 28 cha Sheria ya Chakula, Dawa na Vipodozi sura ya 219, inazuia mtu yeyote kuzalisha, kuingiza, kusambaza na kuuza nchini chakula kilichofungashwa kabla ya kusajiliwa na mamlaka.
TFDA katika ripoti hiyo ilifafanua kuwa vyakula ambavyo havijafungwa kama matunda na nafaka hukaguliwa kwa kuchukuliwa sampuli, ambazo hufanyiwa uchunguzi wa kimaabara na uchanganuzi wa madhara yanayoweza kutokea.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili ulibaini kuwa katika mitaa mingi ya Jiji la Dar es Salaam, wafanyabiashara hao husaga unga wa mahindi na kuuweka katika vifungashio vya kilo tano, 10, na 25.
Msemaji wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Roida Andusamile, alisema jukumu lao ni kusimamia bidhaa zilizopo sokoni kwa kukagua ubora wake, lakini wanapata wakati mgumu kwa wafanyabiashara ambao wapo vichochoroni na wanakwepa kufuata utaratibu kwa makusudi.
Aliongeza kuwa kila bidhaa ambayo wameikagua ina nembo ya ubora au mhuri wao, kitu ambacho ni rahisi hata kwa walaji au watumiaji kutoa taarifa pindi wanapoona bidhaa haina mhuri huo.
Kwa mujibu wa uchunguzi wa gazeti hili, wasagaji wa unga wamekuwa hawafuatia sheria inayowakataza kuzalisha bidhaa zao kwenye mazingira machafu.
Mtaalamu wa chakula wa TFDA, Kyaruzi Jason alisema kuwa bado wana kazi kuwafikia wananchi hasa wasindikaji wadogo kutokana na kukosekana kwa ushirikishwaji wa sekta nyingine.
Alisema hakuna mpangilio maalumu wa maeneo ya viwanda, hali inayowafanya washindwe kuwafikia wasindikaji wote, hasa walio maeneo ya vichochoroni.
Madhara ya unga huo
Uchunguzi unaonyesha kuwa baadhi ya unga huo umeanza kuleta madhara kwa watumiaji, ikiwemo kusababisha ugonjwa wa kuhara. Wengine hushindwa kuutumia kwa sababu una ladha chungu, wenye rangi nyeusi kwa mbali na harufu mbaya.
“Usinunue kwenye duka la hapo kona nunua katika duka la mbele hilo unga wake ni mchungu na mweusi,” alisikika mama mmoja akimuonya mwanaye.
Gazeti hili lilifanya uchunguzi katika baadhi ya mashine za kusaga za Jiji la Dar es Salaam hasa maeneo ya Mbagala, Manzese na Tandale na kushuhudia mahindi yakiingizwa katika mashine ya kusaga bila ya kuondolewa uchafu.
Uchunguzi ulibaini baadhi ya mashine hizo zipo katika mazingira ya uchafu, ikiwemo mifereji ya maji machafu kupita karibu na mashine hizo, pia maeneo yalipo mahindi hayo kuhifadhiwa bidhaa nyingine kama mafuta ya taa, dawa za kuulia wadudu, sabuni na bia.
Mbali ya kuhifadhiwa katika mazingira mabaya mwandishi wa habari hii alishuhudia baadhi ya wasindikaji wakisaga mahindi hayo bila ya kuangalia kama kuna mawe, mabaki ya magunzi wala takataka nyingine.
Godfrey Kibatwe, mkazi wa Mbagala jijini Dar es Salaam ambaye ni mmoja wa vijana wanaofanya kazi kwenye moja ya mashine za kusaga nafaka zilizopo katika eneo hilo, alisema wao kazi yao siyo kusafisha mahindi bali ni kusaga na kuweka kwenye vifungashio kulingana na makubaliano yao na mwenye mashine.
Alisema kazi ya kuondoa uchafu katika mahindi yanayosubiri kuingia kwenye mashine ni kubwa, hivyo inahitaji vibarua ambao wanalipwa na mwenye mahindi.
Kibatwe alisema wanachofanya wao ni mahindi hayo au nafaka nyingine kuipitisha kwenye chekeche kutoa vumbi na kama kuna uchafu mwingine huwa hawauangalii.
Omari Mtagwa ni kijana ambaye hufanya kazi za kusaga unga maeneo ya Mabibo jijini Dar es Salaam, alisema kuwa wao husaga kulingana na makubaliano na tajiri ambapo tani moja husaga kwa kiasi cha Sh30,000 au 40,000 kulingana na uwezo wa tajiri lakini haiwi chini ya hapo.
Alisema bei hiyo ni tofauti na kusaga na kukoboa ambapo kukoboa ni Sh20,000 kwa tani moja ambayo ni sawa na kilo 1,000, kazi ambayo huifanya kwa siku nzima.
Kijana aliyejitambulisha kwa jina moja la Prosper anauza duka maeneo ya Tandika, ambapo dukani kwake kuna unga wa aina tatu na bei tatu tofauti. Upo wa Sh1,400, 1,300 na 1,100, namuuliza sababu za kuwepo aina hizo tatu za unga anasema kuwa ni kutokana na kutofautiana ubora ambapo huo wa bei kubwa ni mweupe hata ukiutizama tofauti na wa Sh1,100.
“Hata tunaponunua kwa wauzaji wa jumla kuna wa bei nafuu na wa bei kubwa kulingana na ubora wake kwa macho na kwa kuukamata mkononi, kwa kuwa tumeuza siku nyingi tunajua, na ndiyo maana hata sisi tunauza bei tofauti,” alisema Prosper.
Kijana mwingine anayefanya kazi hiyo Tandika Kwa Maguruwe jijini Dar es Salaam aliyejitambulisha kwa jina moja la Bob, alisema kuwa kazi hiyo ni ngumu na inahitaji nguvu sasa kama watafanya na kazi ya kuchambua uchafu kutoka katika mahindi hayo itachukua muda mrefu kuimaliza.
“Kazi hii inatofautiana kulingana na tajiri, wengine wapo makini na wanaweka watu wa kuyamwagia maji kabisa, lakini wengine hawana huo mpango na sisi tunafanya kulingana na wao wanavyotulipa, wakitulipa vizuri na kuwa makini kama hao wengine kwa nini tufanye kazi mbaya,” alisema.
Bob alikiri kuwa hata yeye amewahi kula unga ambao ulikuwa na wadudu, lakini kwa kuwa anajua tatizo lipo wapi hakuwa na sababu ya kumlaumu mwenye duka zaidi ya kuwaambia wana familia wake wahame na kununua katika duka lingine.
Alisema utofauti wa ubora wa unga unatokana na mahindi anayoleta tajiri yaani anayetaka kusagiwa na maelekezo yake, kuna ambaye anataka yapitishwe kwenye mashine kama ada badala ya kukobolewa sana na kuna anayeagiza yakobolewe sana na kuajiri wapetaji ambao hupeta kwa usimamizi maalumu.
Profesa George Shumbusho wa Chuo Kkuu cha Mzumbe Morogoro, alisema kuwa sheria nyingi zilizopo hazifanyiwi kazi kutokana na kuingiliwa na wanasiasa.
“TBS wana dhamira na sheria zao lakini tatizo ni utekelezaji wake kutokana na miundombinu, lakini vile vile sheria nyingi zinaingiliwa na wanasiasa kwa mfano kuna maeneo hao wasindikaji wadogo wamewekwa na viongozi ambao wanahitaji kupata kura kutoka kwao, hivyo inakuwa ngumu utekelezaji kwani hawa wanaweza kusema hivi wale wakasema vile,” alisema Profesa Shumbusho.
Dk Raymond Mwenekano wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, anayataja madhara ya ulaji wa vyakula vilivyoandaliwa bila uangalizi maalumu kuwa ni kupata magonjwa kama vile kansa ya utumbo, mwili kuwasha, kubabuka na vidonda mwilini.
“Madhara yake ni makubwa, ndiyo maana siku zote tunasisitiza kula vyakula vilivyoandaliwa kwa umakini na uangalizi maalumu ili kuepuka madhara kama hayo ambayo mara chache huwa ya muda mfupi lakini mara nyingi huwa ni ya muda mrefu na ni vigumu mtumiaji kujua kuwa hayo madhara aliyapata kwa kula vyakula hivyo,” alisema Mwenekano.

No comments:

- See more at: http://www.helperblogger.com/2012/06/jquery-facebook-like-box-popup-with.html#sthash.AGJhd6Gy.dpuf