
Historia na utendaji wa vyama vya siasa nchini inaonyesha kuwa mara baada ya kuanzishwa, vyama vya upinzani, kwa ujumla wake vilikuwa dhaifu. Ni kweli kulikuwa na NCCR-Mageuzi ambayo iligeuka kuwa tishio kiasi kwamba baadhi ya watu wakadhani ndiyo ingeweza kukimaliza Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Hata hivyo, baada ya muda, NCCR-Mageuzi ikafifia na kuiacha CCM ikiendelea kutamalaki.
Baadaye kikaibuka Chama cha Wananchi (CUF) na
kuichachafya CCM hadi baadhi ya watu wakaamini kuwa ndiyo ule ukombozi
wa kweli wa Mtanzania kutoka chama hicho tawala ambacho kimekuwa
madarakani tangu kupatikana kwa uhuru. Nayo ikafifia na kuiacha CCM
ikiendelea kutawala.
Labda hicho kilikuwa kipindi cha mpito. Kilikuwa
ni kipindi cha vyama kujifunza jinsi ya kuendesha siasa za vyama vingi.
Kumbuka kuwa kabla ya hapo waliokuwa wanaendesha vyama vya upinzani
walikuwa hawana uzoefu wa kuwa wapinzani. Hivyo, walikosa maarifa ya
kukabiliana na siasa, mikakati, propaganda na sera za chama tawala.
Baadaye kikaubuka Chama cha Demokrasia na
Maendeleo (Chadema). Kikaja kwa kasi sana kiasi kuwa wakati fulani
ilifikia hatua badala ya wapinzani kuwa wanajibu mapigo ya CCM, chama
hicho tawala ndicho kikageuka kuwa ndicho kinajibu kutoka kwa Chadema.
Bado Chadema inaendelea na kazi hiyo kama
tunavyoshuhudia hivi sasa kwenye mchakato wa kuandika Katiba Mpya ambapo
kwa mara ya pili Rais Jakaya Kikwete amelazimika kukutana nao ili
kuweka sawa baadhi ya mambo katika mchakato huo.
Ukiangalia kwa makini kuibuka kwa Chadema na nguvu
hizo utabaini kuwa si nguvu zake pekee, kwa kiasi kikubwa, udhaifu wa
CCM yenyewe umechangia kukidhoofisha na kuifanya Chadema iibuke kwa
nguvu.
Kuna sababu kadhaa zilizokidhoofisha CCM na nyingi
ya sababu hizo ni za ndani. Inaelekea ilifika wakati chama hicho
kikajisahau, hasa baada ya wapinzani kuibuka na kuzama na kudhani kuwa
hakuna mpinzani ambaye anaweza kukiletea madhara.
Hali hii ikakifanya chama hicho na viongozi wake
kubweteka. Ikatoa nafasi kwa Chadema, ambayo ilikuwa imeshajifunza
kupitia makosa ambayo yalifanywa na watangulizi wake, kuishika CCM
barabara.
Lakini pia kulikuwa na migogoro ndani ya CCM
iliyozalishwa na vita vya madaraka. Wengi wanadhani kuwa migogoro hii
imeanza siku za karibuni lakini ukichunguza kwa undani utabaini kuwa
asili ya migogoro hii ni tangu kuteuliwa kwa Benjamin Mkapa kuwa mgombea
wa chama hicho mwaka 1995. Wakati huo, ambapo ilikuwa imepita miaka 10
tangu Mwalimu Julius Nyerere kung’atuka kwenye uongozi, wengi
walishaweka tamaa ya kuchukua nafasi hiyo.
Hata hivyo, hawakujua kuwa bado Nyerere alikuwa na
uwezo mkubwa wa kuathiri uamuzi ndani ya chama. Kilichotokea wakati wa
uteuzi mwaka 1995 kiliwafanya waanzishe harakati na mikakati ya chini
kwa chini ndani ya chama ili kuhakikisha kuwa inapofika wakati wa uteuzi
mwingine hawapigwi chini. Ndiyo njia ambayo ilitumiwa na Rais Kikwete.
Kwa muda mrefu, tangu Rais Kikwete kuingia
madarakani, hata uongozi ndani ya chama ulishindwa kutulia na kufanya
kazi ya siasa kutokana na migogoro hii. Hivi sasa hali inaelekea
kutengemaa baada ya kuteuliwa kwa Abdulrahman Kinana kuwa Katibu Mkuu wa
chama hicho.
Hata watumishi wengine ndani ya chama wanakiri kuwa kuteuliwa
kwa Kinana kumehuisha chama hicho kwa sababu hivi sasa kazi si tu
zinafanyika, bali zinaonekana kufanyika. Wakizungumza kwa masharti ya
kutotajwa majina yao wanabainisha kuwa kama si umahiri wa Kinana, hivi
sasa Chadema kingekuwa imekifikisha CCM mahali pabaya.
“Kuna wakati kazi za chama zilikuwa zinafanywa
kwa kuzingatia nadharia za kwenye vitabu kuliko hali halisi. Matokeo
yake chama kikaanza kupoteza mvuto kwa watu wa kawaida. Lakini
tunashukuru hivi sasa kuwa CCM kimerejea kwenye nafasi yake kama chama
cha kutetea wanyonge,” anabainisha mfanyakazi mmoja kutoka Makao Makuu
ya CCM, Dodoma.
Tangu kuteuliwa kwake miezi kadhaa iliyopita,
Kinana tayari ameshafanya ziara katika zaidi ya nusu ya mikoa yote
Tanzania Bara. Ziara hizo zimemwezesha kuona kwa uhalisia matatizo
yanayokikabili chama hicho na hivyo kuwa katika nafasi nzuri zaidi ya
kutafuta ufumbuzi wake.
“Unapozunguka huku vijijini unapata nafasi ya
kujionea na kusikia moja kwa moja kutoka kwa wanachama kuhusu matatizo
wanayokabiliana nayo… kama ukikaa ofisini tu na kusubiri ripoti za
watendaji kila siku utakuwa unaongopewa tu,” anasema Kinana.
Katika mahojiano hayo, Kinana anasisitiza kuwa
uhai wa chama kwa kiasi kikubwa unategemea wananchama. Anasema kuna
makosa yanafanyika ndani ya chama kwa viongozi kudhani kuwa chama ni
ngazi za uongozi.
“Wasichokifahamu viongozi wengi ni kuwa katika
ngazi za juu za chama hakuna wanachama… hakuna wanachama kwenye
halmashauri kuu ya taifa, hakuna wanachama kwenye ngazi ya mkoa na
wilaya. Wanachama wapo kwenye shina. Huko ndiko ambako tunapaswa
kukutilia mkazo,” anasema.
Anawataka viongozi wa mikoa na wilaya wasikae tu
ofisini na kusubiri ripoti kutoka ngazi ya chini. Wanapaswa kutoka
ofisini na kutembelea mashina ambako watakutana na wanachama.
Katika ziara yake ya karibuni iliyomchukua siku
18, akiambatana na Katibu wa Uenezi na itikadi, Nape Nnauye, Kinana
amekuwa akiwakemea viongozi wa Serikali ambao wamekuwa na tabia ya
umangimeza na uzembe wa kushughulikia matatizo ya wananchi.
Kimsingi, Kinana anabainisha kuwa kuna viongozi wa
serikali ambao wanaonekana kuwa wamesahau kuwa wanapaswa kutekeleza
sera za CCM ambayo ndiyo iliyoiunda Serikali wanayoitumikia.
Kinana alitumia ziara hiyo kuwaonya watendaji hao
wabovu na kuwataka kuacha tabia ya umangimeza. Alisema CCM kimekuwa
kikilaumiwa kutokana na kukwama kwa miradi mingi ya maendeleo lakini
ukichunguza kwa umakini utabaini kuwa katika maeneo mengi kukwama huko
hakutokani na mipango mibaya, bali uzembe wa watendaji wa serikali
kutekeleza mipango iliyopo kwa ufanisi.
Mathalan, akiwa katika kijiji kimoja katika jimbo
la Solwa mkoani Shinyanga, msafara wake ulisimamishwa na wanakijiji
waliokuwa wanalalamika kwa nini hawapati maji safi wakati bomba kubwa la
maji kutoka Ziwa Victoria linapita hapo.
Alipowauliza viongozi wa mkoa waliokuwa
wameandamana nao, Kinana aliambiwa kuwa kuna mradi mwingine wa kusambaza
maji katika vijiji vinavyopitiwa na bomba hilo. Fedha kwa ajili ya
mradi huo zilikuwa zimetolewa na kuwa utekelezaji wake umepangwa kuanza
mwezi ujao.
Wanakijiji waliposikia jibu hilo walishangilia na kumshukuru
Kinana kwa kupita hapo kwani asingepita wasingesikia kuhusu habari hiyo
nzuri kwao.
Haya ni baadhi ya mambo ambayo Kinana anayafanya
ambao yanakirejeshea CCM nguvu yake ambayo ilipotea kutokana na kukomaa
kwa upinzani na kutokana na migogoro ya ndani ya chama. Hata hivyo, hii
haimaanishi kuwa CCM kinavizidi vyama vya upinzani katika medani ya
siasa, kwani vyama hivyo navyo vimekuwa vikiendelea na mikakati yake ya
kuhakikisha kuwa vinaiondoa madarakani kupitia uchaguzi wa serikali za
mitaa mwakani na Uchaguzi Mkuu 2015.
No comments:
Post a Comment