
Likitajwa jina Kariakoo, fikra zitakupeleka kwenye eneo lenye watu wengi, harakati lukuki na hata biashara za aina nyingi, misongamano mikubwa ya watu na magari.
Hata hivyo, kama unaipenda Kariako, jipe fursa ya
kuitembelea ukianzia saa 12 jioni ambako eneo hilo ambalo ni Soko Kuu
lililoko katikati ya Jiji la Dar es Salaam lina vibweka vingi.
Wakati huo jua linapoanza kuzama, joto la mchana
kutwa nalo likapungua, msongamano wa magari unazidi, usafiri unakuwa wa
taabu kwa kila mmoja anayenuia kurejea nyumbani mapema.
Ifikapo saa mbili usiku, msongamano unaendelea
kupungua, idadi ya watu nayo inapungua na sasa jiji linageuka…watu wengi
wanaelekea katika makazi yao mapya na hata ya zamani.
Kwa mfano, safari za kwenda Mbezi, Tabata,
Vingunguti, Msasani, Kimara, Mbagala zinaongezeka na kuyaacha maeneo
mengi ya katikati ya jiji yakiwa matupu.
Hata hivyo kwa, Kariakoo kuanzia saa tano usiku yapo maisha mapya yanayoanza.
Maisha hayo yana watu wake, mazingira yake, raha zake, upweke wake na shughuli za kila aina ambazo ni wachache wanaozifahamu.
Unapowadia usiku Kariakoo ni jiji jipya kabisa
ambalo ratiba zake huwa ni za kimya zaidi, za umakini na pengine
hazitabiriki wala hazina uhakika wa kufanikiwa au kutokufanikiwa.
Binafsi, ninafika ndani ya Kariakoo saa mbili na
nusu usiku na kukuta shamrashamra zimepungua taratibu mithili ya sauti
ya mvua inayoanza kukatika.
Wafanyabiashara waliojipanga katika mitaa ya
Msimbazi na makutano ya Msimbazi na Uhuru wanasubiri dakika za lala
salama za kupata riziki zao.
Muda huu, vipo vikundi vidogo vidogo vya watu
wanaocheza bao, wanabishana kuhusu mambo mengi yakiwamo mpira hasa wa
Ulaya au hata siasa huku vicheko vya chini chini vikisikika.
Pembeni yupo muuza kahawa na birika lake la moto
linaloendelea kuchemka, huku sinia la kashata likisubiri kusindikiza
kahawa hiyo anayouza.
Mamalishe nao tayari wameanza kufunga vifaa vyao tayari kurejea
majumbani kwao. Magari machache ya abiria nayo bado yanapita hapa na
pale yakimalizia wateja wa mwisho mwisho kwa siku hiyo.
Saa 8:30 usiku, tayari maduka mengi makubwa kwa
madogo yamefungwa, nje katika vibaraza vya maduka hayo taa zinawaka na
humo ndimo vilipo vitanda vya mamia ya Watanzania.
Ninapojongea katika kibaraza kimoja kilichopo Mtaa
wa Swahili ndani ya soko hili la Kariakoo nakutana na macho ya
Watanzania hao wakazi wa vibarazani.
Kuna msururu wa vijana saba katika kibaraza hiki ambao wamelala mbalimbali bila kusogeleana.
Unaweza kupata taswira ya kutisha kidogo
unapowaona kwa mbali kwani wapo katika sare ya mifuko ya salfeti ya
rangi nyeupe, jambo ambalo laweza kukupa picha ya kuogofya kidogo.
Ikiwa tayari imeshafika saa tano sasa, mambo yanazidi kunoga.
Ninamwamsha kijana mmoja aliye katikati ya vijana wenzake karibu saba waliokuwa katika kibaraza hicho.
Anaitika na kusema kuwa anaitwa Mussa Athuman au maarufu kama Mangoronyo.
Mangoronyo anayafikicha macho yake kuondoa
usingizi na ninapomwomba tuzungumze anakubali na mimi ninaketi juu ya
boksi lake ambalo ninabaini hilo ndilo godoro lake kwa miaka 12 sasa.
“Nimekuja hapa Dar es Salaam tangu mwaka 2002
nikitokea Iringa. Nilijua tu kuwa nakuja kutafuta maisha kama ambavyo
nilikuwa nasikia kuwa huku zipo biashara nyingi za kufanya,” anasema
Mangoronyo.
Hata hivyo, Mangoronyo tofauti na matarajio yake anasema hakuweza kupata ajira kama alivyokuwa akiota.
Badala yake alikaribishwa na wimbi la vijana wenye
roho ngumu, waliomwibia baadhi ya nguo zake na fedha kidogo
alizokujanazo kutoka kwao Iringa.
Ikabidi nami nijifunze kuishi kisela kama nilivyowaona wenzangu. Nilipewa orodha ya ajira ninazoweza kufanya, kama kuuza maji, karanga, sigara na pipi, mifuko ya plastiki, lakini pia sikukosa kuambiwa kuwa naweza kudokoa vitu na kupata hela nyingi,” anasema.
Ikabidi nami nijifunze kuishi kisela kama nilivyowaona wenzangu. Nilipewa orodha ya ajira ninazoweza kufanya, kama kuuza maji, karanga, sigara na pipi, mifuko ya plastiki, lakini pia sikukosa kuambiwa kuwa naweza kudokoa vitu na kupata hela nyingi,” anasema.
Mangoronyo hakuwa na pa kulala wala pa kula na
hivyo maisha yake yakawa Kariakoo. Hadi sasa anaishi katika eneo hilo,
anakula na kulala Kariakoo.
Fedha anayopata baada ya kufanya vibarua vya
kubeba mizigo au kuuza chupa tupu za maji, humtosheleza kwa kula tu,
lakini si kuwa na nyumba ya kuishi.
Inapofika jioni, mamia ya vijana hawa wenye makazi
yasiyo rasmi katikati ya jiji, huanza kutafuta maboksi ya kulalia
ambayo nayo huuzwa.
Wapo watu ambao huyapata maboksi hayo kutoka kwa wenye maduka na kuyauza kwa bei ya Sh100 hadi 200.
Kauli ya Manispaa Ilala
Afisa Habari wa Manispaa ya Ilala, Tabu Shaibu
alisema suala hili ni pana mno hivyo anahitaji kuzungumza na kujadili
kwa kina na kitengo cha ustawi wa jamii.
Makazi ya kibaraza kwa Sh500
Katika kibaraza kilichopo Mtaa wa Pemba na Swahili, yupo Awedi Athuman ambaye ametokea Songea, Ruvuma tangu mwaka 2008.
Anasema alitoroka nyumbani kwao akidhani jijini
humu (Dar es Salaam) kuna raha na kazi za kufanya zenye mishahara
minono, lakini alipofika alimezwa na jiji kubwa linalopendeza lakini
lenye mzigo wa dhiki.
Athuman alijikuta akilipia karibu kila kitu
ambacho anafanya katika jiji hili. Alitakiwa kulipia kibaraza
anacholalia kwa bei ya Sh500.
Kibaraza anacholala kijana huyu kipo katika duka la Osama na malipo hutakiwa kwenda kwa Mzee Kassim, mlinzi wa duka hilo.
“Nilishinda na njaa, kiu mpaka nikaanza kuombaomba, lakini
nikagundua kuwa kuombaomba nikiwa nina viungo vyangu hakuna maana.
Nikaanza kujiajiri kwa kuwasaidia watu kubeba mizigo yao na wananipa
hela,” anasema.
Fedha kidogo anayoipata kijana huyu huishia katika mlo ambao waweza kuwa ni mmoja au akibahatisha miwili kwa siku.
Anatakiwa kuoga, jambo ambalo nalo linahitaji
fedha: “Kuoga ni Sh300, kujisaidia 200, yaani sikuwahi kudhania katika
maisha yangu kuwa hivyo vitu vinalipiwa, yaani hata kujisaidia,” anasema
Athuman kwa mshangao.
Anasema siku akikosa hela basi huzibana haja zake
kwa sababu ya hali halisi ya Kariakoo ambayo hakuna mahali pa kujibanza
ili ujisaidie.
Mifuko ya salpheti ni shuka
Ndani ya soko hilo, vile unavyodhani wewe kuwa ni
taka basi kwa wakazi wa Kariakoo usiku ni bidhaa. Vijana wengi wanaolala
katika vibaraza hivi hutumia mifuko ya salpheti kama mashuka yao.
Ni kama sare. Kwani utaukuta msururu wa watu waliojipanga katika kibaraza wote wakiwa na mifuko hii miguuni hadi kiunoni.
Hata hivyo, wapo pia ambao wamekosa mifuko hiyo na hulala na nguo zao tu huku mbu wakiifaidi miili yao.
Licha ya maisha haya, wengi wanaolala Kariakoo usiku wana vitu wanavyomiliki kama nguo, viatu na mswaki.
Kwa mfano, Shariff Mussa amelala juu ya boksi lake lakini kichwani amelalia mto ambao ni begi la nguo zake.
Ndani ya begi hilo kuna mswaki, mashati mawili, matatu na karatasi ambayo ameandika namba za simu za ndugu zake walioko Mbeya.
“Nimesoma mpaka darasa la pili. Ninachokijua ni
kuandika, nasoma kwa tabu sana, lakini nipo hapa natafuta maisha, siku
nikifanikiwa nadhani nitakuwa na makazi yangu,” anasema Mussa.
Anaongeza kuwa ametumia vibaraza vya Kariakoo kama vyumba vya
kulala kwa miaka mitatu sasa tangu alipotoka Kijiji cha Mlalo, Mbeya
mwaka 2011.
Kubakwa, kurubuniwa na wahuni
Shariff mwenye umri wa miaka 19 anasema, alikuja
akiwa mdogo na ameshuhudia vijana na watoto wadogo wakirubuniwa kwa
ajili ya kupata riziki.
Anasema, watoto wa mitaani ambao wamekuja kutoka
vijijini na wanaishi katika maeneo ya Kariakoo baadhi yao hurubuniwa na
kulawitiwa na vijana wakubwa katika soko hilo.
“Ni tamaa au kudanganywa. Wanafanyiwa vitendo vya
ajabu ajabu hapa na wakati mwingine tunashuhudia. Inasikitisha,” anasema
Mussa.
Siri ya mifuko inayobeba chupa tupu za maji
Mangoronyo anaeleza kuwa Kariakoo hakuna urafiki zaidi ya salamu au ugomvi.
Hata hivyo, wakazi wa usiku wa kariakoo hawanyimani mbinu.
Mbinu hizo ni zile zinazobuniwa kila siku kuhusu jinsi ya kuiba au kufanya uhalifu fulani.
Mangoronyo anasema, wengi wanaookota chupa tupu za
maji, wakati mwingine huiba ‘side mirror’ za magari au taa na
kuzitumbukiza katika mifuko hiyo kisha kuendelea na shughuli kana kwamba
hakuna kilichotokea.
“Si rahisi kuhisi kuwa mifuko hiyo ina kitu zaidi ya chupa za maji,” anasema.
No comments:
Post a Comment